Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Yakobo UTANGULIZI

UTANGULIZI
Waraka huu wa Yakobo hauzungumzii sana masuala ya Kitheolojia, ila lengo lake ni kuwahimiza na kuwatia moyo walengwa wake wawe watekelezaji wa neno la Mungu na sio wasikilizaji tu (1:22). Waraka huu ni mwongozo wa maadili unaolenga jumuiya zote za Kikristo ambazo zinatajwa kwa jina moja la mfano kama: “Makabila kumi na mawili yaliyotawanyika” (1:1).
Waraka huu una mengi yanayofanana na maandishi ya hekima. Hekima ambayo ni karama kutoka kwa Mungu inachukua nafasi muhimu katika fikira za Yakobo (1:5; 3:13-18). Kuwa na hekima si kuwa na ujuzi mkuu wa mambo ya sayansi, elimu ya ubinadamu au ya kimungu bali ni kutenda mema (4:17) “kwa mwenendo wake mzuri” (3:13) kulingana na matakwa ya Mungu. Katika 2:1-5, ile desturi au tabia ambayo inawapendelea matajiri na kuwaweka maskini pembeni lazima ikomeshwe na kukataliwa. Wakristo walipata kudhalilishwa na matajiri wasio Wakristo (2:6-7). Wafanya biashara matajiri wanaonywa kwamba matumaini yao ya kuwa salama siku za baadaye hayana msingi (4:13-17). Wanaotajirika kwa kujiwekea mishahara ya haki ya wafanya kazi wao watahukumiwa (5:1-6).
Yakobo anazitaka jumuiya za Kikristo zingojee kwa uvumilivu kuja kwake Bwana (5:7-11). Waumini wanatakiwa kusali pamoja (5:13), wazee wa kanisa wanatakiwa wawaombee wagonjwa na kuwapaka mafuta maana maombi ya namna hiyo huponya na kuleta msamaha wa dhambi (5:14-15). Katika 5:16-19 waumini wanatakiwa kuungamiana dhambi zao na kufanya bidii kumrudisha yeyote miongoni mwao aliyetenda dhambi (5:20).
Katika kuwahimiza waumini washikilie maadili ya Kikristo, Yakobo anaonekana kukumbuka mahubiri ya Yesu hasa Hotuba Mlimani (Mt 5-7) kuhusu imani kamilifu (1:22-25; 2:14-16; 3:13-18), kuhusu kukabili majaribu kwa uvumilivu (1:2-4,12-15; 5:7-11), kuhukumu kwa huruma (2:12-13; 4:11-12), kuutawala ulimi (1:26; 3:1-12), kuepa kuapa (5:12) na kudumu katika sala (5:13-18).

Iliyochaguliwa sasa

Yakobo UTANGULIZI: SRUV

Kuonyesha

Shirikisha

Nakili

None

Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia

YouVersion hutumia vidakuzi kubinafsisha matumizi yako. Kwa kutumia tovuti yetu, unakubali matumizi yetu ya vidakuzi kama ilivyoelezwa katika Sera yetu ya Faragha