YouVersion Logo
Search Icon

Zaburi 71

71
Mungu tumaini la wazee
1Kwako ee Mwenyezi-Mungu, nakimbilia usalama;
kamwe usiniache niaibike!
2Kwa uadilifu wako uniokoe na kunisalimisha;
unitegee sikio lako na kuniokoa!
3Uwe mwamba wangu wa kukimbilia usalama,
ngome imara ya kuniokoa,
kwani wewe ni mwamba na ngome yangu.
4Niokoe, ee Mungu wangu, mikononi mwa waovu,
kutoka makuchani mwa wabaya na wakatili.
5Maana wewe Bwana u tumaini langu;
tegemeo langu ee Mwenyezi-Mungu, tangu ujana wangu;
6nimekutegemea tangu kuzaliwa kwangu,
ndiwe uliyenitoa tumboni mwa mama yangu.
Mimi nitakusifu wewe daima.
7Kwa wengi nimekuwa kioja,
lakini wewe u kimbilio langu imara.
8Kinywa changu kimejaa sifa zako,
na utukufu wako mchana kutwa.
9Wakati wa uzee usinitupe;
niishiwapo na nguvu usiniache.
10Maana maadui zangu wanasema vibaya juu yangu;
wanaovizia uhai wangu wanafanya mipango,
11na kusema: “Mungu amemwacha;
mfuateni na kumkamata,
kwani hakuna wa kumwokoa!”
12Usikae mbali nami, ee Mungu;
uje haraka kunisaidia, ee Mungu wangu.
13Wapinzani wangu wote waaibishwe na kuangamizwa;
wenye kutaka kuniumiza wapate aibu na fedheha.
14Lakini mimi nitakuwa na matumaini daima;
tena nitakusifu zaidi na zaidi.
15Kinywa changu kitatamka matendo yako ya haki,
nitatangaza mchana kutwa matendo yako ya wokovu
ijapokuwa hayo yanapita akili zangu.
16Nitataja matendo yako makuu, ee Bwana Mwenyezi-Mungu;
nitatangaza kuwa ndiwe mwadilifu peke yako.
17Ee Mungu, wewe umenifunza tangu ujana wangu;
tena na tena, natangaza matendo yako ya ajabu.
18Usiniache, ee Mungu, niwapo mzee mwenye mvi,
hata nivitangazie vizazi vijavyo nguvu yako.
19Nguvu na uadilifu wako, ee Mungu,
vyafika mpaka mbingu za juu.
Wewe umefanya mambo makuu mno.
Ee Mungu, ni nani aliye kama wewe?
20Umenifanya nione taabu nyingi ngumu,
lakini utanirudishia tena uhai,
wewe utaniinua tena kutoka huko chini.
21Utaniongezea heshima yangu,
na kunifariji tena.
22Nitakusifu pia kwa kinubi,
kwa sababu ya uaminifu wako, ee Mungu wangu;
nitakuimbia sifa kwa zeze, ewe Mtakatifu wa Israeli.
23Nitapaza sauti kwa furaha,
ninapokuimbia wewe sifa zako,
na roho yangu itakusifu maana umeniokoa.
24Nitatamka uadilifu wako mchana kutwa,
maana waliotaka kuniumiza wameaibishwa na kufedheheshwa.

Currently Selected:

Zaburi 71: BHN

Highlight

Share

Copy

None

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in

YouVersion uses cookies to personalize your experience. By using our website, you accept our use of cookies as described in our Privacy Policy