YouVersion Logo
Search Icon

Methali 31

31
Mawaidha kwa mfalme
1Maneno ya mfalme Lemueli. Mawaidha aliyofundishwa na mama yake:
2Nikuambie nini mwanangu?
Nikuambie nini mwanangu niliyekuzaa?
Nikuambie nini wewe niliyekuomba kwa Mungu?
3Usimalize nguvu zako kwa wanawake,
usiwape mali yako hao wanaoangamiza wafalme.
4Haifai ee Lemueli, haifai wafalme kunywa divai,
wala wakuu kutamani vileo.
5Wakinywa watasahau maagizo ya sheria,
na kuwanyima haki wenye taabu.
6Mpe kileo mtu anayekufa,
wape divai wale wenye huzuni tele;
7wanywe na kusahau umaskini wao,
wasikumbuke tena taabu yao.
8Lakini wewe, lazima useme kwa ajili ya wote walio bubu;
na kutetea haki za wote wasiojiweza.
9Sema kwa ajili yao na kuamua kwa haki,
linda haki za maskini na fukara.
Mke mwema
10Mke mwema kweli, apatikana wapi?
Huyo ana thamani kuliko johari!
11Mumewe humwamini kwa moyo,
kwake atapata faida daima.
12Kamwe hamtendei mumewe mabaya,
bali humtendea mema maisha yake yote.
13Hutafuta sufu na kitani,
na kufanya kazi kwa mikono yake kwa bidii.
14Yeye ni kama meli za biashara:
Huleta chakula chake kutoka mbali.
15Huamka kabla ya mapambazuko,
akaitayarishia jamaa yake chakula,
na kuwagawia kazi watumishi wake.
16Hufikiria kununua shamba, kisha hulinunua,
na kulima zabibu kwa faida ya jasho lake.
17Huwa tayari kufanya kazi kwa nguvu
na kuiimarisha mikono yake.
18Hutambua kwamba shughuli zake zina faida;
hufanya kazi hata usiku kwa mwanga wa taa yake.
19Husokota nyuzi kwa mikono yake mwenyewe,
kwa vidole vyake mwenyewe husuka nguo zake.
20Huufungua mkono wake kuwapa maskini,
hunyosha mkono kuwasaidia fukara.
21Hawahofii watu wake ijapo baridi ya kipupwe,
maana kila mmoja anazo nguo za kutosha.
22Hujitengenezea matandiko,
mavazi yake ni ya zambarau ya kitani safi.
23Mume wake ni mtu mashuhuri barazani,
anakoshiriki vikao vya wazee wa nchi.
24Mwanamke huyo hutengeneza nguo na kuziuza,
huwauzia wafanyabiashara mishipi.
25Nguvu na heshima ndizo sifa zake,
hucheka afikiriapo wakati ujao.
26Hufungua kinywa kunena kwa hekima,
huwashauri wengine kwa wema.
27Huchunguza yote yanayofanyika nyumbani mwake,
kamwe hakai bure hata kidogo.
28Watoto wake huamka na kumshukuru,
mumewe huimba sifa zake.
29Husema, “Wanawake wengi wametenda mambo ya ajabu,
lakini wewe umewashinda wote.”
30Madaha huhadaa na uzuri haufai,
bali mwanamke amchaye Mwenyezi-Mungu atasifiwa.
31Jasho lake lastahili kulipwa,
shughuli zake hazina budi kuheshimiwa popote.

Currently Selected:

Methali 31: BHN

Highlight

Share

Copy

None

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in

YouVersion uses cookies to personalize your experience. By using our website, you accept our use of cookies as described in our Privacy Policy