YouVersion Logo
Search Icon

Yeremia 6

6
Yerusalemu imezingirwa na maadui
1Enyi watu wa Benyamini,
ondokeni Yerusalemu mkimbilie usalama!
Pigeni tarumbeta mjini Tekoa;
onesheni ishara huko Beth-hakeremu,
maana maafa na maangamizi makubwa
yanakuja kutoka upande wa kaskazini.
2Mji wa Siyoni ni mzuri na mwororo,
lakini utaangamizwa.
3Watu wataujia kama wachungaji na makundi yao,
watapiga hema zao kuuzunguka kila mmoja sehemu yake,
wapate kuyaongoza makundi yao.
4Watasema: “Jitayarisheni kuushambulia Siyoni.
Haya! Tuanze kushambulia adhuhuri!
Bahati mbaya; jua linatua!
Kivuli cha jioni kinarefuka.
5Basi, tutaushambulia usiku;
tutayaharibu majumba yake ya kifalme.”
6Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema:
“Kateni miti yake,
rundikeni udongo kuuzingira Yerusalemu.
Mji huu ni lazima uadhibiwe,
maana hamna lolote ndani yake ila dhuluma.
7Kama kisima kinavyohifadhi maji yake yakabaki safi,
ndivyo Yerusalemu unavyohifadhi uovu wako.
Ukatili na uharibifu vyasikika ndani yake,
magonjwa na majeraha yake nayaona daima.
8Hilo na liwe onyo kwako ee Yerusalemu,
la sivyo nitakutupa kabisa kwa chuki;
nikakufanya uwe jangwa,
mahali pasipokaliwa na mtu.”
Watu wasiopenda kusikia
9Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema hivi:
“Kusanyeni watu wote wa Israeli waliobaki
kama watu wakusanyavyo zabibu zote;
kama afanyavyo mchumazabibu,
pitisheni tena mikono yenu katika matawi yake.”
10Nitaongea na nani nipate kumwonya,
ili wapate kunisikia?
Tazama, masikio yao yameziba,#6:10 yameziba: Kiebrania: Hayajatahiriwa.
hawawezi kusikia ujumbe wako.
Kwao neno lako, ee Mwenyezi-Mungu,
limekuwa jambo la dhihaka,
hawalifurahii hata kidogo.
11Nimejaa hasira ya Mwenyezi-Mungu dhidi yao.
Nashindwa kuizuia ndani yangu.
Mwenyezi-Mungu akaniambia:
“Imwage hasira barabarani juu ya watoto
na pia juu ya makundi ya vijana;
wote, mume na mke watachukuliwa,
kadhalika na wazee na wakongwe.
12Nyumba zao zitapewa watu wengine,
kadhalika na mashamba yao na wake zao;
maana nitaunyosha mkono wangu,
kuwaadhibu wakazi wa nchi hii.
Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
13Wote, tangu mdogo hadi mkubwa kabisa,
kila mmoja anatamani kupata faida isiyo halali.
Tangu manabii hadi makuhani,
kila mmoja wao ni mdanganyifu.
14Wameliponya jeraha la watu wangu juujuu,
wanasema; ‘Amani, amani’,
kumbe hakuna amani yoyote!
15Je, waliona aibu walipofanya machukizo hayo?
La! Hawakuona aibu hata kidogo.
Hawakujua hata namna ya kuona aibu.
Kwa hiyo wataanguka pamoja na wale waangukao;
wakati nitakapowaadhibu,
wataangamizwa kabisa.
Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”
Israeli akataa njia ya Mungu
16Mwenyezi-Mungu asema hivi:
“Simameni katika njia panda, mtazame.
Ulizeni mjue juu ya matukio ya zamani.
Tafuteni mahali ilipo njia nzuri
muifuate nanyi mtapumzisha nafsi zenu.
Lakini wao wakasema:
‘Hatutafuata njia hiyo.’
17Kisha nikawawekea walinzi, nikawaambia:
‘Sikilizeni ishara ya tarumbeta.’
Lakini wao wakasema: ‘Hatutaisikiliza.’
18“Kwa hiyo, sikilizeni enyi mataifa;
enyi jumuiya ya watu jueni yatakayowapata.
19Sikiliza ee dunia!
Mimi nitawaletea maafa watu hawa
kulingana na nia zao mbaya.
Maana hawakuyajali maneno yangu,
na mafundisho yangu nayo wameyakataa.
20Ya nini kuniletea ubani kutoka Sheba,
na udi wa harufu nzuri kutoka nchi ya mbali?
Sadaka zenu za kuteketezwa hazikubaliki,
wala tambiko zenu hazinipendezi.
21Kwa hiyo mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi:
Tazama, nitawawekea watu hawa vikwazo
ambavyo vitawakwaza na kuwaangusha chini.
Akina baba na watoto wao wa kiume wataangamia,
kadhalika na majirani na marafiki.”
Mashambulizi kutoka kaskazini
22Mwenyezi-Mungu asema hivi:
“Tazameni, watu wanakuja toka nchi ya kaskazini;
taifa kubwa linajitayarisha kutoka mbali duniani.
23Wamezishika pinde zao na mikuki,
watu wakatili wasio na huruma.
Vishindo vyao ni kama ngurumo ya bahari.
Wamepanda farasi,
wamejipanga tayari kwa vita,
dhidi yako ewe Siyoni!”
24Waisraeli wanasema,
“Tumesikia habari zao,
mikono yetu imelegea;
tumeshikwa na dhiki na uchungu,
kama mwanamke anayejifungua.
25Hatuwezi kwenda mashambani,
wala kutembea barabarani;
maadui wameshika silaha mikononi,
vitisho vimejaa kila mahali.”
26Mwenyezi-Mungu asema,
“Jivikeni mavazi ya gunia, enyi watu wangu
na kugaagaa katika majivu.
Ombolezeni kwa uchungu,
kama mtu anayemwombolezea mwana wa pekee,
maana mwangamizi atakuja,
na kuwashambulia ghafla.
27Yeremia, wewe nimekuweka kuwa mchunguzi
na mpimaji wa watu wangu,
ili uchunguze na kuzijua njia zao.
28Wote ni waasi wakaidi,
ni watu wanaopitapita wakisengenya wengine,
wagumu kama shaba nyeusi au chuma;
wote hutenda kwa ufisadi.
29Mifuo inafukuta kwa nguvu,
risasi inayeyukia humohumo motoni;
ni bure kuendelea kuwatakasa watu wangu,
waovu hawawezi kuondolewa uchafu wao.
30Wataitwa ‘Takataka za fedha’,
maana mimi Mwenyezi-Mungu nimewakataa.”

Currently Selected:

Yeremia 6: BHN

Highlight

Share

Copy

None

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in

YouVersion uses cookies to personalize your experience. By using our website, you accept our use of cookies as described in our Privacy Policy